Sunday, December 10, 2006

Prof. Ishengoma: Si lazima wote twende bungeni

Diwani msomi anayeongoza Kata ya Mbuyuni Morogoro
-Asema wanawake wasifungiwe kwenye chupa
-Vijana wengi wa Kitanzania awaita 'broilers'
na innocent munyuku
NI asubuhi ya saa mbili na nusu hivi. Jumamosi iliyotulia, siku ambayo nimejaa shauku ya kukutana na msomi aliyebobea katika masuala ya kilimo lakini akaamua kuwania nafasi ya chini katika siasa.
Huyu si mwingine bali ni Profesa Romanus Ishengoma (54), Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine Morogoro ambaye hivi karibuni iliyopita amefanya mahojiano maalumu na RAI na kutoboa kisa cha yeye kujiingiza katika siasa akiwania nafasi ya chini kabisa.
Akiwa amevalia vazi la kaptula na shati la bluu ananifuata katika lango kuu la kuingilia nyumbani kwake eneo la Falkland mjini Morogoro. Ananikaribisha baada ya utambulisho mfupi. Ni mwingi wa mazungumzo lakini kila anachozungumza hasiti kukitolea mifano na wakati mwingine kukushirikisha katika mazungumzo kwa kuuliza maswali.
ÒUnaujua huu ni mti gani?Ó ananiuliza akinionyesha mti mmojawapo unaopendezesha nyumba yake iliyozungukwa na mti. Mti huo anaouliza ni wa aina ya cacao ambao kwa mazoea haulimwi nchini Tanzania.
Lakini baadaye ananieleza kuwa anaelewa fika kwamba si kwenda kuangalia miti aliyoipanda na hivyo ananipisha niendelee na kiini cha safari yangu.
Nami bila kusita namjibu kwamba kilichonileta ni habari ya miti pia kwa hiyo hana haja ya kuacha kuzungumzia suala la mazingira. Tunashirikiana kicheko na kuketi katika viti nje ya nyumba yake.
Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana, wengi hawakuelewa pale waliposoma kwenye magazeti au kupata habari kupitia vyombo vingine kwamba Profesa wa Chuo Kikuu anawania nafasi ya udiwani wa Kata ya Mbuyuni mjini Morogoro.
Prof. Ishengoma analielezea jambo hilo kuwa ni msimamo wake katika maisha.
ÒSiwezi kuwa driven (kuendeshwa) na mkumbo, na hii ni kwa sababu nina elimu ambayo ndio msingi mkubwa wa maisha.
ÒKusema tu kwamba mimi ni profesa haitoshi, mchango wangu ni nini katika jamiiÉmaendeleo daima huanzia katika grass roots na huu ndio mchango,Ó anasema na kisha kuongeza:
ÒKwa hiyo unapozungumzia udiwani unazungumzia msingi wa mambo mengi ya jamii, na labda niwakumbushe wanaonishangaa kwamba udiwani hauniondelei uprofesa nilionao.Ó
Anasema aliona ni vema aanzie na udiwani kwani ipo haja ya kujenga msingi.
ÒNawashauri wasomi au niseme maprofesa wenzangu, tuache kulalamika na badala yake tuanze kuwaletea maendeleo wananchi sehemu tunazoishi.
ÒLakini hapa pia tuwekane sawa kwamba si lazima wote twende bungeni. Maprofesa wamebaki kulalamika na wengi hawataki kuwatumikia wananchi,Ó anasema.
Je, katika uchaguzi huo wa mwaka jana hakutengwa na wananchi wa Morogoro kwa ukabila hasa ikizingatiwa kwamba yeye ni mtu wa Bukoba?
ÒWananchi wa Morogoro si wakabila, naomba tusiwapakazie. Lakini niliwahi kusikia minongÕono juu ya jambo hilo. Lakini hawa mimi ni ndugu zangu.
ÒHili nalisema kwa uwazi kabisa, Waluguru ni ndugu zangu. Nimekaa hapa kwa miaka zaidi ya 30 na sioni kama natengwa kama wapo wenye hulka hiyo ni wachache. Sasa hatuwezi kusema Waluguru ni wakabila wakati wenye tabia hiyo si wengi.Ó
Anazungumziaje Serikali ya Rais Jakaya Kikwete hasa katika kipindi hiki cha kuelekea mwaka mmoja madarakani?
Prof. Ishengoma ambaye Januari 19 mwaka huu alichaguliwa kuwa Meya wa Manispaa ya Morogoro anasema Kikwete kaanza vizuri katika uongozi wake.
ÒHuu mwaka mmoja wa Kikwete vya kusifiwa ni vingi kuliko lawama, kuna kasi ya maendeleoÉkuna attitude ya uwajibikaji kwa viongozi.
ÒAmekuwa Rais ambaye hakai chini katika utendaji. Sasa kama Rais anakosa muda wa kupumzika wewe wa chini utalalaje?Ó anahoji Prof. Ishengoma.
Anasema pia katika nyanja za kiusalama, Serikali ya Kikwete imefanya jitihada na imefanikiwa kupunguza nguvu za ujambazi.ÒUsalama wa raia upo ingawa sehemu za Magharibi bado kuna tatizo.Ó
Lakini je, vipi kuhusu tatizo la umeme linalowakabili Watanzania na uchumi wao? Prof. Ishengoma anasema si jambo jema kumtupia lawama Rais Kikwete pekee.
ÒTusimtafute mchawi, hili suala la umeme lina uhusiano mkubwa na mazingira. Sisi tunazalisha umeme wa maji, watu wanaharibu mazingira unategemea nini?
ÒHatuna reserves za majiÉlazima tujifunze kutunza mazingira na hili si la kuzembea kabisa ni vizuri kuvisaidia vyanzo vya maji.
ÒMimi nipo Morogoro tangu mwaka 1973 wakati huo kulikuwa na maji yanatiririka milimani na hata marehemu Mbaraka Mwinshehe aliimba. Leo hii hakuna kitu kama hicho. Tuwajibike sasa kwa pamoja.Ó
Anapozungumzia suala la Tanzania kujiunga na Jumuiya ya Afrika Mashariki, anasema Watanzania hawana haja kuwa waoga na muungano huo.
ÒNi kweli tuna suala la Muungano wetu na Zanzibar ambalo linasumbua kidogo, lakini huwezi kukataa Jumuiya kwa kigezo cha Zanzibar.
ÒTunatakiwa kuelewa kuwa kuna mambo ya bed room (chumba cha kulala) na sitting room (sebuleni) sasa mazungumzo ya vyumba ni tofauti kabisa.
ÒKuleta hoja ya woga hapa huu ni ujinga na hatuwezi kusema kuwa hatuendi huko. Sisi kama nchi hatuwezi kukwepa mabadiliko. You change or changes will change you. Mimi naona tusisubiri mabadiliko yatubadilishe ni heri tubadilike sasa,Ó anasema na kuongeza:
ÒDunia inakwenda na wakati kwa njia ya muungano. Sasa kama dunia inaungana sisi tunasubiri nini?
ÒSuala hapa basi liwe ku-survive na tujiulize how do we join. Je, tunakubaliana nini huko? Tunafanyaje? Lakini isiletwe hoja ya kipuuzi kwamba tukwepe kuungana. Tutakwisha.Ó
Anaongeza kuwa jambo la msingi katika Jumuiya ya Afrika Mashariki ni kuangalia Tanzania inapeleka kitu gani sokoni. Anasema kwa mfano kama Wakenya wana uhaba wa mahindi ni jukumu la Watanzania kulima mahindi na kuyasambaza katika soko la Kenya.
ÒMbona leo hii tunakula apples za Afrika Kusini? Hapa sasa tuangalie nafasi yetu kisoko na si kukwepa muungano huu.Ó
Mbali na kuungwa kwake Jumuiya ya Afrika Mashariki, Prof. Ishengoma ni mtu wa karibu anayependa kuona wanawake wanapewa nafasi katika jamii.
Anasema si jambo jema kuwafungia wanawake kwenye chupa. ÒWape uhuru waonyeshe vipaji vyao na tuache dharau dhidi yao.Ó
Lakini kuna jambo jingine linalomkera sana. Nalo ni vijana kupotoka kimaadili. Anasema vijana wengi wanataka kuwa Wamarekani; hawautaki Utanzania.
ÒWako brain washed kabisa lakini wameharibiwa na sinema wanadhani kuwa hayo ndiyo maisha halisi. Vijana hawa ni kama kuku broilers, sisi tunataka kuku wa kienyeji.Ó
Katika maisha ya kawaida, Prof. Ishengoma ametumia elimu yake ya misitu kuyatengeneza mazingira ya makazi yake.
Kuna miti mbalimbali mojawapo ni cacao ambao wengi wanaamini kuwa miti hiyo haiwezi kustawi hapa nchini. Ana miti aina ya mdalasini, miembe na bwawa la samaki.
Kimsingi hakuna zao la bustani ambalo utalikosa kwa Prof. Ishengoma na anajivunia jambo hilo na kwamba amefanya hivyo kupunguza gharama za maisha.
ÒLitakuwa ni jambo la ajabu sana kama nitakwenda sokoni au mtu wa familia yangu anakwenda sokoni kutafuta nyanya, ndizi au pilipili. Nina kila kitu humu ndani,Ó anasema Prof. Ishengoma.
Profesa Ishengoma alizaliwa mkoani Kagera Aprili 4, 1952 alikopata elimu yake ya msingi kabla ya kujiunga na sekondari ya Nyakato mkoani Mwanza.
Alimaliza kidato cha sita katika Shule ya Sekondari ya Mazengo mkoani Dodoma mwaka 1972 na mwaka uliofuata Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kampasi ya Morogoro ambayo baadaye ndiyo ilizaa SUA.
Mwaka 1986 alipata udaktari wa sayansi ya kilimo kutoka Chuo Kikuu cha Kilimo cha Norway na mwaka 1996 akawa profesa kamili. Msomi huyo ambaye yuko kazini kwa miaka 30, mke wake ndiye Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Dk. Christine Ishengoma.

Zemkala, Machifu, Maembe na Usiku wa Umoja

na innocent munyuku

MKUSANYIKO wa muziki wa reggae, midundo ya ngoma za asili kutoka kwa kundi la Zemkala na Bagamoyo Pirits ni mambo yanayoanza kulitikiza jiji la Dar es Salaam kiasi cha wiki mbili zilizopita.

Pengine niseme kuwa mashabiki wa muziki wamezoea mkusanyiko kama huo kuwa kwenye matamasha maalumu na si mazoea ya kila wiki. Lakini sasa hilo limewezekana baada ya Umoja Entertainment kuanzisha Usiku wa Umoja unaofanyika kila Ijumaa kwenye Ukumbi wa Art Gallery Mbezi Beach jijini Dar es Salaam.

Ni usiku wa mseto wenye kila aina raha kwa mashabiki wa muziki. Naam ndivyo ulivyo kutokana na mchanganyiko wa vipaji wasanii wa aina mbalimbali. Kuanzia wataalamu wa reggae, ngoma za asili na Madj wenye ujuzi wa kuwarusha mashabiki kwa staili nyingine za muziki kwa mtindo wa disko.

Lakini ukiachana na muziki wa Dj, cha kufurahisha ni mkusanyiko wa vichwa vyenye ujuzi wa muziki. Hawa ndio wasanii halisi waliopikwa wakapikika na wamedhihirisha hilo katika ulimwengu wa medani hiyo katika kona nyingi za dunia.

Tuanze na kundi la Zemkala. Hawa ni vijana wananane waliojikusanya kwa nia ya kuzinadi ngoma za asili. Zemkala ni neno la Kiyao likiwa na maana ya maendeleo.

Lije jua au mvua Zemkala hawana masihara kwenye kazi na ndio maana katika Usiku wa Umoja huko Art Gallery mashabiki wanapagawa kwa staili yao ya uimbaji na uchezaji wa ngoma za asili.

Kundi hilo linawajumuisha Yuster Nyakachara, Havintishi Baraza, Fadhili Mkenda, Yusuf Chambuso, Maulid Mastir, Kasembe Ungani, Shabaan Mugado na Fred Saganda.

Unapopigwa wimbo wa Tuvine (Tucheze) waweza kudhani kuwa jukwaa linasambaratika muda huo kutokana na kishindo kikuu cha ngoma za vijana hao ambao hawajavuka umri wa miaka 30.

Katika onyesho la Ijumaa iliyopita wakati mwendesha shughuli alipotangaza kuwa Zemkala walikuwa wanajiandaa kuvamia jukwaa na midundo ya asili, baadhi ya mashabiki pengine kwa ile dhana ya kubeza muziki wa utamaduni walianza minongÕono ya kutoridhika.

Lakini baada ya kundi hilo kuanza kuonyesha umahiri wao, hapakuwa na kuangalia pembeni zaidi ya kuwakodolea macho wasanii hao na kuwasindikiza kwa vifijo na nderemo. Huo ukawa ushindi kwa Zemkala dhidi ya fikra potofu zinazojali muziki wa kigeni.

Kabla ya Zemkala, kulikuwa na onyesho kutoka kwa Bagamoyo Pirits linaloongozwa na msanii kinara Vitali Maembe ambaye Jumamosi hii anamalizia stashahada yake kwenye Chuo cha Sanaa cha Kimataifa cha Bagamoyo.

Kama ilivyotarajiwa, Maembe na kundi lake wakiwa na mtindo wao wa Motokaa, waliwakumbusha mashabiki uhondo wa kibao cha Sumu ya Teja na hivyo kuwateka nyoyo mashabiki.

Ukiachana na hao, wengine waliokamilisha Usiku wa Umoja ni kundi la reggae la Machifu. Kazi ya wasanii hawa kwa hakika iliwashangaza wengi kutokana na ukweli kwamba si kundi linalofanya mazoezi ya pamoja.

Kila mmoja yu katika pilika zake na ikifika siku ya onyesho kila muhusika hukumbatia majukumu yake jukwaani na si rahisi kujua kuwa hawako pamoja katika mazoezi ya kila siku.

Wanapoimba kibao cha Julia moja kwa moja kutoka jukwaani si rahisi kujua watu hawa hawana mazoezi ya muda mrefu katika maisha yao. Hukutana saa chache kabla ya onyesho.

Ni wanamapinduzi, waliojaa fikra za kumkomboa mtu Mweusi kutoka kwenye makucha ya watu wa Magharibi. Makucha ambayo kwa miaka mingi yameendelea kuwaumiza Waafrika kwa kisingizio cha ustaarabu.

Hawa ni wakombozi wanaotumia magitaa, vinanda na sauti zao katika kuwalaani mafisadi wanaendelea kuikandamiza nafsi ya mnyonge si ndani ya Afrika tu bali duniani kote kunakohubiriwa upendo.

Lakini nini hasa kiini cha kuleta Usiku wa Umoja? Mwasisi wa usiku huo, Gotta Warioba ameliambia gazeti hili kuwa lengo ni kuwapa mashabiki mseto wa burudani.

ÒHili wazo ni la muda na nimekuwa nikiwaza kuwa kuna umuhimu wa kuwa na kitu kama hiki kwa sababu bila mkusanyiko wa aina hii hatuwezi kufika mbali.

ÒUmekuwa shahidi hapa. Wasanii wamepiga reggae, ngoma za asili na huu ni mwanzo tu nadhani katika siku zijazo tutakuwa na ladha tofauti tofauti zaidi,Ó anasema Gotta.

Lakini mbali na kuwakusanya mashabiki kwa lengo la kuonyesha uwezo wao, Gotta anasema huo ni mwanya kwa vikundi kuendelea kuwa katika joto la jukwaa kila leo.

Anasema si jambo zuri kwa msanii kusubiri mialiko ya msimu wakati upo uwezo wa kuwakutanisha kila wiki. Kwamba mbali na kubadilishana mawazo, mkusanyiko kama huo ni sawa na kisima cha ujuzi kwa wasanii.

Je, wasanii wenyewe wanasemaje kuhusu Usiku wa Umoja? Maembe anaeleza kuwa amefarijika kutokana na utaratibu huo kwa sababu mbali na kujitangaza, wanapata fursa ya kuona mwamko wa mashabiki dhidi ya kazi za sanaa.

Kauli kama hiyo haina tofauti sana na Kasembe Ungani wa Zemkala. ÒTumekuwa tukisubiri sana mambo kama hayaÉhapa unazidi kuwa mwenye hamu ya kuendelea na sanaa kwa sababu unapata changamoto za kila aina.Ó

Lakini kwa mujibu wa Ungani changamoto pia kwa watu wengine wanaojitangaza kuwa wasanii wakati hawana ubunifu wowote.

ÒSisi hapa umeona tunapiga kazi moja kwa moja hakuna anayetumia CD kuimba, watu wanapiga vyombo kwa ubunifu mkubwa. Hii ndiyo tofauti na hao wengine,Ó anaeleza.

Anasema kutokana na hilo ni vema wanaodhani kuwa wasanii wakajipanga upya kwani kuimba pasipokujua upigaji wa ala mbalimbali na elimu ya muziki kwa ujumla ni kujidanganya.

Kwa mtazamo wangu, usiku huu usiwe kama mbio za sakafuni. Wasanii pamoja na waandaaji waendelee kulitangaza jina la sanaa kwa ubora unaosubiriwa na mashabiki.

Ni wazi kuwa kama mjumuiko wa aina hiyo utaendelea kuimarishwa, wasanii watakuwa na nafasi nzuri ya kujiimarisha katika kazi zao za kila siku kwani umoja daima ni nguvu.

Umoja una umuhimu mkubwa katika maisha ya mwanadamu na hilo limewekwa kwenye maandiko ya Biblia na Quran pia. Kwamba tuwe na umoja ili kujenga uhusiano mwema daima.

munyuku@gmail.com
0754 471 920

Kirigini: Serikali ya Tanganyika itarudi

na innocent munyuku

HERMAN Kirigini si jina geni katika ulimwengu wa siasa nchini Tanzania. Ameshaliwakilisha bungeni jimbo la Musoma Vijijini kuanzia mwaka 1975 hadi 1985. Hivi karibuni mkongwe huyo wa siasa amezungumza na RAI katika mahojiano maalumu kuhusu mustakabali wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na kagusia Muungano na kurejeshwa kwa Serikali ya Tanganyika.

Akizungumzia juu ya mchakato wa Shirikisho la Mashariki, Kirigini anasema kimsingi watawala wa nchi zote tatu yaani Kenya, Uganda na Tanzania wamewaburuza wananchi wake.

Kwa mtazamo wake, nchi kama Tanzania inaburuzwa kuingia katika muungano huo na kwamba rais wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa anastahili lawama kwa kuridhia jambo hilo.

“Huyu wa kwetu niseme kwa uwazi kabisa aliburuzwa. Ndiyo! Mkapa aliburuzwa kwa sababu alikuwa dhaifu,” anasema na kuongeza kuwa Tanzania inakimbilia huko pasipo kujua udhaifu wao kiuchumi.

Anasema kuwa kwa kasi ya ukuaji wa uchumi unaofanywa na Kenya ni wazi Tanzania itamezwa katika jumuiya hiyo.

Kwamba Tanzania na Uganda si ajabu zikawa dampo la bidhaa kutoka Kenya kutokana na takwimu za mwaka uliopita juu ya bidhaa zinazouzwa nje ya nchi.

Mwaka jana, Kenya iliiuzia Tanzania na Uganda bidhaa mbalimbali za viwandani zenye thamani ya dola za Marekani milioni 593.351 wakati Tanzania na Uganda zikiiuzia Kenya bidhaa zenye thamani ya dola za Marekani milioni 186.200.

Katika mwaka huo huo, Uganda na Tanzania ziliagiza kutoka Kenya bidhaa zenye thamani ya dola za Marekani milioni 638.992 na hii kwa mtazamo wa Kirigini nchi hizi hazina uwezo sawa kiushindani.

“Uchumi wa Tanzania na Uganda unategemea zaidi kilimo cha mazao wakati ule wa Kenya ukitegemea viwanda na huduma,” anasema Kirigini na kisha kuongeza:

“Hali hii inaufanya uchumi wa Kenya kuwa imara zaidi kushinda wa Tanzania na Uganda unaotegemea hali ya hewa wakati ule Kenya ambao daima unategemea uzalishaji wa bidhaa za viwandani.”

Lakini pia Kirigini anasema kuwa nchi hizi tatu katika suala la mapato na bajeti zake kwa mwaka hayalingani. Kwamba Kenya inapata dola bilioni 3.715 na matumizi yao ni dola 3.88.

Tanzania inapata dola za Marekani bilioni 2.235 huku matumizi yake yakiwa dola 2.669. Uganda inapata dola bilioni 1.845 na inatumia dola bilioni 1.904 kwa mwaka.

“Ndiyo maana nasema wananchi wanaburuzwa na viongozi wa kisiasa katika jambo hili,” anasema.

Hata hivyo, anasisitiza kuwa hili suala la watu kutangaza kutaka maoni juu ya wananchi kuhusu shirikisho ni hadaa kwani maamuzi yalishafanywa.

“Leo hii unawauliza wananchi inasaidia nini? Hii ni hadaa, wangepewa nafasi ya kwanza kutoa maoni. Hivi kweli hatukumbuki tulivyoumia baada ya Jumuiya ya awali iliyovunjika mwaka 1977? Nani walifaidika zaidi kama sio Wakenya?”

Anasema wakati jumuiya inavunjika njia kuu za uchumi zilikuwa zikishikiliwa Kenya na wao wakaziendeleza kwa maslahi yao.

“Tuliumwa na nyoka na je, leo tuna uhakika gani kama muungano huu hautavunjika?” anahoji Kirigini.

Akizungumzia suala la Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, Kirigini anaeleza kuwa Rais Jakaya Kikwete ameachwa peke yake.

“Kikwete analia peke yake katika kutatua mgogoro wa kisiasa Visiwani na kasoro za Muungano. Hawa viongozi wa CCM hawampi ushirikiano kukemea maovu ya Zanzibar.

“Kasimama bungeni (Kikwete) na kusema kuwa kuna mpasuko wa kisiasa Zanzibar lakini mbona hawamsaidii kuyakemea?

“Zanzibar kuna tatizo kubwa sana, Karume ni sawa na Salmin Amour wanalewa madaraka.”

Anasema kutokana na kasoro hizo ipo siku hoja ya Serikali ya Tanganyika itaibuka upya.

“Mimi nasema Serikali ya Tanganyika lazima itarudi na kosa alilofanya Nyerere ni kutokubali kubaki na Tanganyika, amefariki dunia akilijua hilo na hakuweza kurudi nyuma,” anasema Kirigini.

“Lakini mbali na jambo hilo, jambo jingine ni kwamba wengi waliomfuata Nyerere walikuwa wanafiki, walimwogopa badala ya kumshauri.

“Mimi sikutaka kuwa katika mkumbo huo na ndio maana wakati fulani bungeni nilichachamaa kwa kuwatetea wakulima wa pamba.

“Hili si Bunge, nakumbuka katika utetezi wangu kwa wakulima, Mwalimu alitaka kunikamata, alidai mimi na wenzangu tunapinga chama ndani ya Bunge.”

Anasema alichofunza katika miaka yake kama mwanasiasa ni kwamba CCM haitaki kuukubali upinzani na kutokana na misimamo yake, wana-CCM wengi wamekuwa wakimtenga kwa kumwona msaliti.

“Mwaka 1987 niliomba ujumbe wa NEC nikapewa alama ya E na kwamba mimi ni msaliti wa kisiasa, nikaandika barua Halmashauri Kuu lakini hadi hii leo sijajibiwa.

“Nikaonekana mbaya kwa watu wa mkoa wangu lakini upinzani ule leo hii ndio huo ambao umekubalika. Kuna chama kama CUF ni vema kikaendelea kuwepo ili pawe na criticism.”

Anaeleza kuwa mawazo makongwe hasa kutoka kwa baadhi ya wanasiasa wasiokubali mabadiliko yamesababisha CCM wakati mwingine kukosa mwamko.

“Lakini bado nakubali kwamba hawa walioko CCM baadhi yao wakitoka na kuunda chama kingine chama hicho kitakuwa bora kwani wapinzani wa kweli wangali humo.”

Kuhusu mwaka mmoja wa Serikali ya Kikwete, Kirigini anaeleza kuwa mtawala huyo anakubalika na wengi lakini kasi yake wengi hawaiwezi.

“Kikwete ana kasi ya ajabu na mtu mzuri lakini watu wake (viongozi) hawaendi naye. Wameachwa nyuma na kama mpiganaji, anatakiwa arudi nyuma aangalie majeshi yake mfano ni hizi Serikali za Mitaa zimeoza.”

Hata hivyo, anapingana na utaratibu wa Serikali kuwachangisha wananchi kwa ajili ya sherehe za Uhuru. Anasema kimsingi ni heri jambo hilo likawa katika bajeti.

“Waliochanga wengi ni wafanyabiashara na kwa kawaida wafanyabiashara hawana nia nzuri, wanakuwa na lao jambo.”

Kirigini ambaye kitaaluma ni Bwanashamba alizaliwa Desemba 22, 1955 ameoa na ana watoto wanane mmoja kati ya hao ni Rosemary Kirigini ambaye ni Mbunge wa Viti Maalumu (CCM).

Kirigini amewahi kuwa Waziri wa Mifugo kati ya mwaka 1980-83 na kati ya mwaka 1983-85 akawa Waziri wa Nchi anayeshughulikia mifugo.

Amewahi pia kuwa Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga na Arusha kati ya mwaka 1993-96. Ana shahada ya kilimo aliyoipata Chuo Kikuu cha Makerere mwaka 1970.

Raila kapiga zumari Kenya, tulicheze Tanzania

na innocent munyuku

WANASEMA uzee ni dalili ya hekima lakini pamoja na ukweli huo uzee hauhalalishi kuziba vipaji au mianya ya wengine kuonyesha uwezo wao katika masuala mbalimbali yahusuyo jamii. Basi tuseme pia katika hili uzee waweza kutumika kama mwongozo au mifano sahihi kwa ustawi wa jamii.

Katika hilo ndio maana hadi hii leo kwa baadhi ya kaya huwatumia wazee katika kufanya suluhisho kwenye eneo husika hasa kama kutatokea kutokuelewana baina yao. Pengine kutokana na hilo inawezekana wengine wakadiriki kusema kuwa ukubwa ni jalala.

Lakini katika nyanja za siasa hasa barani Afrika hali ni tofauti. Wazee wameonyesha njia mbaya kwa kung’ang’ania madaraka na huu kwa mtazamo wa kawaida kabisa ni ishara na mwongozo usiofaa kwa vijana wanaochipukia katika siasa na hata waliosimama kabisa.

Nimeamua kuandika haya kwa kusimamia hoja ya Mbunge wa Jimbo la Lang’ata nchini Kenya, Raila Odinga aliyependekeza hivi karibuni kuwa ni vema wanasiasa wa nchini mwake ambao wamekuwa madarakani kwa muda mrefu waachie ngazi na kupisha damu changa.

Odinga alisema kuwa anashangaa kuwaona wanasiasa wa jinsi hiyo ambao hadi hii leo wangali wakishika utawala tangu enzi ya marehemu baba yake Jaramongi Oginga Odinga.

Ingawa Odinga alikuwa akiyasema hayo kukipigia debe chama chake cha Orange for Democratic Movement-Kenya (ODM-K), maneno yake yalitosha kuwa changamoto kwa ajili ya kujenga vyama vyenye damu mpya na mawazo mapya katika siasa.

Nchini humo kwa mfano, Makamu wa Rais Moody Awori ana umri wa miaka 79, huku kukiwa na mawaziri wengine wenye umri mkubwa kama yeye akiwemo Njenga Karume (80), Simone Nyachae (75) na John Michuki (74).

Kimsingi hoja ya Raila si ya kuachwa ipite hivi hivi pasipo kuungwa mkono na katika hili ndio maana nasema kuwa mwanasiasa huyo machachari amelenga sehemu husika kutokana na ukweli kwamba sehemu mbalimbali barani Afrika lina tatizo kama hilo.

Tanzania kama ilivyo Kenya pia ina wanasiasa ambao leo hii wana rekodi ya kubakia katika ulingo huo huku wakiziba ya damu changa zisiweze kuonyesha upeo wao katika nyanya mbalimbali. Hao wamejaa tele na ni kama wamepigiliwa misumari.

Ndani ya Tanzania wapo wanasiasa ambao tangu wengine hatujazaliwa wapo katika ulingo huo wakiendesha maisha yao kwa mgongo wa siasa na hadi hii wangali madarakani kama vile hakuna Mtanzania kijana mwenye uwezo wa kuyatenda hayo ayatendayo huyo aliyeko madarakani.

Naungana na Raila kusema kuwa hii ni dalili mbaya kwa mustakabali wa taifa letu kwani ukweli ni kwamba wanasiasa wa aina hii hawana jipya katika mioyo yao. Hawana jipya la kutueleza, wamebaki na mbinu za kale ambazo kwa nyakati hizi hatuwezi kukubaliana nazo.

Kwamba hawana fikra pevu tena, vichwa vyao pamoja na kwamba wanaweza kuwa na hekima, hawana jema la kuwafundisha wengine. Ni heri kwao wakakubali mabadiliko kuliko kung’ang’ania siasa. Huu uwe wakati wa kuwafundisha wengine. Na kufundisha kuzuri ni kwa kumpisha mwanafunzi kitini na kumwelekeza namna ya kuliongoza jahazi.

Kama wanasiasa wa jinsi hii wameshindwa kuleta maendeleo au kuishauri Serikali husika kwa kipindi cha miaka 20 au 30 leo hii watakuwa na miujiza gani katika kulisukuma gurudumu mbele gurudumu la maendeleo na tija halisi kwa Watanzania?

Hawa wazee wa siasa wana jipya gani leo hii? Watasimama waseme kitu ambacho kwa wakati huu watu watakubali kuwa wanachokinena ndicho sahihi? Lakini hakuna shaka kwamba salamu wamezipata wakati ule wa kampeni za Uchaguzi Mkuu mwaka jana. Baadhi yao nasikia walizomewa na wakalazimika kushuka jukwaani wakiwa wamevaa sura za aibu.

Hivi kwani ni lazima wote wawe wanasiasa? Kwanini wengine wasibaki pembeni na kuangalia vichwa vingine vikiongoza jahazi? Bila shaka zumari la Raila lafaa lisikizwe kwa makini na lichezwe hapa kwenye ardhi yetu ya Tanzania. Tusipuuze kwani alichokisema nchini Kenya ndicho kilichopo hapa kwetu.

Sileti siasa za kibaguzi lakini kwa mtazamo, ufike wakati wazee wakubali mabadiliko si kwa kuwapiga watoto wao (wa damu) bali pia kuwapa nafasi wengine wajaribu kujiwekea rekodi zao. Ninachotarajia kwa muda huu ni hawa wazee wajenge vitalu bora kwa kuwapika vijana kisiasa badala ya kuwawekea vizingiti ambavyo kimsingi vinaliangamiza taifa.

Kwamba wakati huu uwe mwafaka kwa Watanzania kujifunza kutokana na changamoto ya kina Raila na kundi lake. Kwani hawa vijana wasipojifunza leo watapata wapi nafasi hiyo? Wasipojaribu leo watajaribu lini?

Tusione aibu kuwapisha vijana waonyeshe walichonacho kwenye vichwa vyao na kama watateleza huo utakuwa muda mwafaka kuwarekebisha na kuwaelekeza wapite wapi na watufikishe wapi. Kuwabana ni kuwanyima haki yao na huu si utaratibu mzuri wa kukuza maendeleo. Tuwape nafasi hii leo.

Niseme pia kuwa hatujachelewa kufikia kuwapa vijana nafasi. Ni suala la maandalizi ambayo yakianza sasa bila shaka katika Uchaguzi Mkuu ujao wazee watakubali kukaa pembeni na kuwapisha vijana waendelee kukimbiza kijiti cha maendeleo.

Hakika tusione aibu kabisa kuanza kulicheza zumari la Raila. Huo ndio uungwana, kubalini mabadiliko mapema ili heshima yenu isipotee.

munyuku@gmail.com